BALOZI WA TANZANIA NCHINI BURUNDI NA BALOZI WA BURUNDI NCHINI TANZANIA WATEMBELEA BMH KUWAJULIA HALI WATOTO WA BURUNDU WALIOFANYIWA UPASUAJI WA MOYO
Na Jeremia Mwakyoma, Gladys Lukindo na Jeremia Mbwambo
DODOMA - JULAI 17, 2026
Balozi wa Tanzania nchini Burundi Mhe. Gelasius Byakanwa na Balozi wa Burundi nchini Tanzania Mhe. Leontine Nzeyimana, kwa pamoja wametembelea Hospitali ya Benjamin Mkapa (BMH) kuwajulia hali watoto kutoka Burundi waliofanyiwa upasuaji wa moyo ambao wanatarajiwa kuruhusiwa wakati wowote kutokea sasa kufuatia Afya zao kuimarika.
Aidha, waheshimiwa mabalozi hao pia waliwajulia hali watoto waliowasili BMH leo wakitokea Burundi ambao nao wamekuja kwa ajili ya huduma hizo za upasuaji wa moyo na kuelezea kuridhishwa na viwango vya huduma wanazopatiwa watoto hao.
Balozi wa Burundi nchini Tanzania Mhe. Leontine Nzeyimana ametoa shukrani za dhati kwa serikali ya Tanzania kwa ushirikiano na Serikali ya Burundi, pia kwa namna ambavyo Mhe Balozi wa Tanzania nchini Burundi anavyoiwakilisha Tanzania jambo lililosaidia kufanikisha kambi ya wiki mbili ya matibabu ya BMH iliyofanyika Burundi mwaka jana 2025 na kusaidia watoto kutoka Burundi kuja BMH kupata matibabu ya upasuaji wa moyo huku akipongeza viwango vya ubora vya BMH.
"Ni mara ya kwanza mimi kufika hapa BMH, nimestaajabu kuona miundombinu ya kisasa iliyopo, tumefahamu kumbe majirani zetu Tanzania wana uwezo mkubwa kwenye sekta ya matibabu, ni jukumu letu sote kusaidiana kuwajulisha wananchi wetu ili wasihangaike kwenda nchi za mbali zenye gharama kutafuta huduma badala yake waje Tanzania" alisisitiza Balozi Leontine Nzeyimana.
Nae Balozi wa Tanzania nchini Burundi Mhe. Gelasius Byakanwa amewapongeza Madaktari na Wataalamu wa BMH naJKCI kuwa huduma waliyoitoa kwa watoto kutoka nchini Burundi imewaheshimisha Watanzania na Taifa kwa ujumla mbele ya nchi majirani.
"Mwanzoni nilipata hofu kama matibabu haya yangewezekana lakini huduma mlizowapatia watoto kutoka Burundi zimerejesha imani kubwa sana kwa nchi yetu mbele ya majirani zetu, serikali imefanya uwekezaji wa hadhi ya kimataifa katika Sekta ya Afya kwa upande wa miundombinu, vifaa tiba na Wataalamu wa kutosha wenye weledi mkubwa" alisisitiza Mhe. Byakanwa.
Aliongeza kuwa kwa mambo aliyoyashuhudia, anaiona BMH miaka 10 au 20 ijayo itakuwa kituo bora cha matibabu kwa Africa, na kuahidi yeye ataendelea kuisemea BMH nje ya nchi huku akitoq wito kwa uongozi wa BMH kutumia maendeleo ya TEHAMA kufikisha elimu ya huduma za kibobezi zinazotolewa Hospitalini hapo kwa wananchi wa mataifa yanayotuzunguka ili kuwasaidia nao kuja kupata huduma hizo BMH kupitia huduma za tiba utalii.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa BMH Prof. Abel Makubi amemshukuru Mhe Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuwekea vizuri mazingira ya Dilpomasia, kupandisha hadhi ya huduma za Afya kuwa za Kitaifa na Kimataifa hali inazozifanya nchi majirani na baadhi ya nchi za Kimataifa kustaajabu juu ya uwezo huo na kupongeza kazi kubwa iliyofanywa na serikali.
Akiwakilisha wazazi wa watoto hao, Bi. Nahimana Concilie amesema awali walihangaika sana kupata huduma hizo bila mafanikio, wanashukuru kuja Tanzania, madaktari wa BMH kwa kuwapokea kwa upendo, kuwapa huduma zenye utaalamu mkubwa na anahamasisha wengine kutoka Burundi kuja BMH.